Search This Blog

UZAZI WA MPANGO HUPONYESHA NA KUSAIDIA WAGUMBA.




NA PETER KATULANDA
KAHAMA.

HUDUMA ya Uzazi wa Mpango ina faida nyingi ikiwa ni pamoja na kuponyesha wanawake wenye matatizo ya maumivu wakati wa hedhi na kusaidia wagumba kupata watoto.
Kutokana na manufaa hayo, akina mama wametakiwa kujiunga na uzazi wa mpango na wanaotumia uzazi huo, kujiepusha na magonjwa ya zinaa ikiwemo kaswende ambayo husababisha madhara kwa wanawake na kuathiri uzazi wa kawaida na wa mpango.
Hayo yamesemwa kwa nyakati tofauti hivi karibuni na Mkufunzi wa Uzazi wa Mpango wilayani Kahama Adventina Kataraiya na mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Kagongwa, iliyopo katika kata ya Asagehe wilayani hapa.
Kataraiya alisema kwamba ugonjwa wa kaswende unaongoza kwa kusababisha madhara ya mimba kwa akina mama wajawazito na kuwa dalili zake hazionekani mapema mpaka anapokuwa mjamzito au anapojifungua.
Aliyataja madhara hayo kuwa ni pamoja na kupata ugumba, kuharibu mimba, kuzaa mtoto mfu, mtoto njiti, mwenye ulemavu, taahira au mtoto kuozea tumboni na kuhatarisha maisha ya mama.
Wataalamu hao walisema kuwa alisema kuwa madhara mengine ya magonjwa hayo kwa baadhi ya wanawake ni kuharibika kwa via vya uzazi na na kuwa si kweli kuwa iwapo wanatumia uzazi wa mpango watapata matatizo ya afya ya uzazi.
Kataraiya alisema, “Madawa ya uzazi wa mpango hayazuii au kutibu magonjwa ya zinaa, ndiyo maana baadhi ya wanawake wanaposhindwa kuzaa au kuharibui mimba, hudhani kuwa ni kwa sababu ya madawa ya uazi wa mpango.”
Alifafanua kuwa “Madawa ya uzazi wa mpango ni salama. Huponyesha wanawake wenye maumivu wakati wa hedhi na kusaidia wagumba, na huweza kuzuia kuanza kwa magonjwa ya kansa kwa wanawake ambao hawajapata ugonjwa huo, na kuwa huweza kusaidia kupata watoto hivyo nawashauri akinamama wenzangu wapimwe na kubaini magonjwa mapema na sio kusingizia dawa za uzazi wa mpango.”
Alidai, kubaini mapema magonjwa na kupata tiba sahihi na ushauri wa matumizi ya uzazi wa mpango na afya ya uzazi, itasaidia kuepuka madhara ya uzazi wa kawaida na uzazi wa mpango.
Alisema njia za uzazi wa mpango zipo za muda mfupi na za muda mrefu zikiwemo za asili na kitaalamu. Njia hizo za kiasili ni unyonyeshaji na kupima ute wa mwanamke ambapo za kitaalamu za muda mfupi ni vidonge vya uzazi wa mpango, sindano na kondomu za kike na kiume.
Njia za muda mrefu ni kitanzi au lupu, vipandikizi na kufunga kabisa uzazi kwa mwanamke na mwanamme ambazo pia hazina madhara yoyote iwapo mtumiaji atafuata masharti na ushauri wa kitaalamu.
“Wanawake wanaotumia njia ya kitanzi wanaweza kupata maambukizi kwa urahisi hivyo wanashauriwa kuzingatiausafi ili kuepuka maambukizi yanayoweza kutokea na kumsababishia kutunga mimba nje ya mfuko wa uzazi.” Alisema mganga mfawidhi Mwaulambo.
Mganga huyo alifafanua kuwa, mama anapofua na kuanika nguo zake anazotumia wakati akiwa hedhi na kuzianika ndani ama chini ya kitanda, ni rahisi kupata maambukizi ya magonjwa kama ya fangas tofauti na yule anayeanika nguo hizo juani na kuzipiga pasi.
“Licha ya kukosa kabisa uzazi, magonjwa hayo ya kaswende au kisonono, humsabisha mwanamke achelewe kubeba mimbana kumuathili kisaikolojia.” Alisema mganga huyo.
Wataalamu hao walitoa wito kwa akina mama kuwahi katika zahanati, vituo vya afya au hospitali ili wachunguzwe maambukizi mbalimbali yakiwemo magonjwa ya zinaa ili kuwaepusha na madhara yatokanayo na maradhi hayo na kuwawezesha kufaidi huduma za uzazi wa kawaida za afya kwa aina mama na uzazi wa mpango.



Mama Kataraiya talking to journalists
MWISHO.